Home » » MAUAJI YA WAKULIMA TENA KITETO

MAUAJI YA WAKULIMA TENA KITETO

MAPAMBANO kati ya wakulima na wafugaji katika Wilaya ya Kiteto mkoani Manyara, yanaendelea kushika kasi na kusababisha watu wanne kupoteza maisha.
Hali hiyo ilibainishwa na Katibu wa wakulima wilayani hapa, Josephat Mponda alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wilayani.
Mponda alisema kuwa usiku wa kuamkia juzi, jamii ya wafugaji wa Kimasai waliwavamia wakulima katika eneo la Lepono na kusababisha mkulima mmoja na wafugaji watatu kupoteza maisha.
Mponda alieleza kuwa kati ya majira ya saa saba na nane usiku, jamii ya wafugaji wa Kimasai waliwavamia wakulima kwa kutumia silaha za moto jambo ambalo lilizua mashambulizi kati ya pande mbili na kusababisha vifo vyawatu hao.
Katibu huyo alisema jamii hiyo ya wafugaji ilivamia maeneo ya Laitini na kuvichoma moto vibanda vya wakulima jambo ambalo lilizua mapambano makali kwa jamii hiyo.
“Kinachoshangaza ni kuwa jamii ya Kimasai inatumia silaha kubwa na nzito huku wakiwa wanajitamba kuwa wanazipata kutoka kwa viongozi na kueleza kuwa watahakikisha wakulima wanaondoka katika maeneo haya ili wabaki wafugaji pekee.
“Lakini cha kushangaza ni Jeshi la Polisi kutokuwa na ukweli katika utoaji wa taarifa kwa wakuu wao wa kazi. Mfano katika mauaji haya yaliyotokea askari wamechukua maiti moja na kuipeleka katika hosptiali ya Kiteto, maiti nyingine tatu wameziacha porini jambo ambalo linaonekana kuficha ukweli wa mambo na kusababisha machafuko kuendelea kuwa makubwa,” alieleza Mponda.
Alisema kuwa iwapo serikali itashindwa kutatua mgogoro huo ambao kwa sasa umechukua miaka mingi, ni wazi kutafikia hatua ya wakulima na wafugaji kuanza vita na Kiteto hakutakalika.
Mkuu wa Polisi Mkoa wa Manyara, Mkilimali Mpwapwa alisema taarifa za awali alizozipata kutoka kwa OCD wa Kiteto ni kuwa mkulima mmoja amefariki na watu watatu wamejeruhiwa.
“Taarifa za awali nilizozipata kutoka kwa OCD ni kuwa mtu mmoja ambaye ni jamii ya wakulima amepoteza maisha na watu wengine watatu wamejeruhiwa na kati ya hao wakulima ni wawili na mfugaji ni mmoja.
“Imeelezwa kuwa walioanza kuvamia wenzao ni wafugaji kwa kuwavamia wakulima na ndipo walipoanza kujibishana kwa kutumia silaha za kijadi  na kusababisha matukio ya mauaji kama hayo na hiyo ilitokea usiku wa kuamkia Jumamosi,” alisema.
RPC Mpwapwa alisema taarifa hizo ambazo amezipata kutoka kwa OCD wake zilikuwa bado hazijawa katika maandishi kutokana na kuendelea kufanya uchunguzi wa matukio hayo.
“Kwakweli matukio ya Kiteto ni ya muda mrefu na yanatakiwa kutatuliwa kwa njia ya kidiplomasia, vinginevyo kunaweza kutokea machafuko makubwa kuliko yaliyopo kwa sasa, kwani ni juzi tu tulikaa na jamii zote za wakulima na wafugaji na tukaongea nao na tukaamini kuwa mambo yamekuwa shwari, lakini cha kushangaza kesho yake ndiyo yanajitokeza mambo kama hayo, jambo hilo ni hatari sana na linaumiza vichwa vyetu,” alisema RPC Mpwapwa.
Alisema mgogoro huo una vyanzo vingi vinavyochochea japo hakuvitaja, lakini kauli hiyo inaweza kuhusishwa na matamko ya Naibu Spika wa Bunge na Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai ambaye alidai kuwa mgogoro huo unakuzwa na ubaguzi wa viongozi pamoja na kuwepo kwa vitendo vya rushwa kwa viongozi hao.
Katika mkutano wa hadhara kati yake na wakulima wa Kiteto, Chemba na Kongwa, Ndugai alisema kuwa mgogoro huo unachangiwa na Mbunge wa Kiteto na Naibu Waziri wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Benedict Ole-Nangoro kwa kuonyesha wazi ubaguzi wa kikabila kati ya wakulima na wafugaji.
Mbali na hilo, Ndugai aliwataja Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi na Mkuu wa Mkoa wa Manyara kuwa ni kati ya viongozi aliodai wanapokea rushwa kutoka kwa wafugaji na kusababisha uamuzi kuwaelemea wakulima ili waondolewe.
Desemba mwaka jana, jamii ya wakulima wapatao wanne walipoteza maisha kutokana na mapigano yaliyozuka kati ya wakulima na wafugaji katika kitongoji cha Olupoponyi anakotokea mbunge Ole-Nangoro.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa