Home » » Ziwa Manyara lipo hatarini kutoweka kabisa kama juhudi hazitachukuliwa kutunza Mazingira

Ziwa Manyara lipo hatarini kutoweka kabisa kama juhudi hazitachukuliwa kutunza Mazingira

Hifadhi ya Taifa ya Ziwa Manyara,ipo hatarini kutoweka iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa kuinusuru.

Mkuu wa Idara ya Ikolojia katika hifadhi hiyo, Christina Kiwango,alitoa taarifa hiyo jana katika kikao maalumu cha Kamati ya Ushauri Mkoa wa Arusha(RCC).

Kiwango alisema kina cha maji cha ziwa hilo,sasa kimepungua na kufikia nusu mita huku pia kila mwaka likikauka kabisa ifikapo Juni.

Alisema kutokana na kukauka maji, ndege zaidi ya milioni mbili aina ya flamingo wamekuwa wakihama kutokana na ukame huo huku pia mamia ya samaki na viboko wakiendelea kutoweka katika hifadhi hiyo.

Alisema hali hiyo inasababishwa na shughuli za kibinadamu hasa kilimo jirani na hifadhi,kuvamiwa maeneo ya mapito ya wanyama na kujengwa makazi kwenye njia za maji na kwenye mapito ya wanyama.

“Kilimo holela kimekuwa tatizo kubwa ambalo linachangia ziwa kujaa tope pia na ufugaji holela ni tatizo na lazima sasa hatua zichukuliwe”alisema Kiwango.

Akizungumzia kupotea hifadhi hiyo,Mwenyekiti wa Halmashauri ya Karatu,Lazaro Maasai alisema kama ikiachwa uchumi wa Wilaya ya Karatu utavurugika sambamba na uchumi wa mji wa Mto wa Mbu na mkoa mzima wa Arusha .

 Alisisitiza kuwapo kwa mpango wa muda mrefu na mfupi ili kunusuru hifadhi hiyo na ziwa hilo kwa manufaa ya uchumi wa mkoa na watu wake.
 

 chanzo-Mwananchi.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa