Home » » Nyumba za wafugaji zachomwa moto

Nyumba za wafugaji zachomwa moto

WAFUGAJI zaidi ya 100 wa jamii ya Kibarbeig wa Kitongoji cha Gidaburuku, Kijiji cha Mulbadau wilayani Hanang’, Mkoa wa Manyara, wanaendelea kuishi porini katika shamba la Gawal baada ya kuchomewa nyumba na maboma yao kupisha ugawaji wa ardhi.
Nyumba hizo zipatazo 24 za wafugaji hao zilianza kuteketezwa wiki iliyopita na kikundi cha wakulima wa kijiji hicho, wakiongozwa na viongozi wa serikali ya kijiji na askari wa Kutuliza Ghasia (FFU).
Kuteketezwa makazi hayo ya wafugaji kumefanyika wiki moja tu tangu Mkuu wa Mkoa, Erasto Mbwilo, kuwataka waondoke kwenye makazi yao kabla ya kuondolewa kwa nguvu ili kupisha ugawaji wa ardhi hiyo ya shamba la Gawal yenye ukubwa wa ekari 4,030.
Wakizungumza na waandishi wa habari wakati wa uteketezaji huo ukiendelea, wafugaji hao walisema licha ya kuchomewa makazi yao pia wamechomewa vyakula na baadhi ya mifugo yao kutawanyika.
Veronica Gidaregek akizungumza akiwa nje ya nyumba ya familia yake iliyoteketezwa, alisema kundi la wakulima likiongozwa na Mwenyekiti wa kijji hicho, Christopher Panga, walivamia nyumba hiyo na kuanza kuichoma moto bila hata kumruhusu kutoa mali zake.
“Mimi sina pa kwenda, nitalala hapa nje na watoto wangu wawili, kwani wamenichomea nyumba na mali zangu zote na mume wangu amesafiri,” alisema Gidaregek.
Nao Mwale Lwagei na Hiyi Hando, walisema wachomaji hao huku wakilindwa na polisi walichoma maboma yao bila hata kuwaelekeza wapi pa kwenda kama nia ni kugawa upya maeneo hayo kwa wananchi wote wa kijiji hicho.
“Kwa kaka yangu, Gidabugai Masungu, walichoma nyumba ndani akiwemo mzazi na nusura wamteketeze kwa moto mtoto mmoja mchanga ambaye tulimuokoa,” alisema Lwagei.
Diwani wa Kata ya Basotu, Samweli Kawoga, alithibitisha kuchomwa makazi na kueleza kuwa shughuli hiyo ilisimamiwa na viongozi wa kijiji cha Mulbadau.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Erasto Mbwilo, jana alisema hakuagiza viongozi wa kijiji hicho wala polisi kuchoma makazi hayo.
“Mimi kwenye ule mkutano nilichoagiza ni wale waliovamia eneo la shamba la Gawal kuondoka ili kupisha ugawaji wa ardhi hiyo, sasa kama kuna watu wamechoma makazi hayo ni makosa na mimi sina taarifa,” alisema.
Naye Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Manyara, Akili Mpwapwa, alisema polisi hawakutumwa kusimamia uchomaji wa makazi bali kusimamia upimaji wa ardhi ya eneo hilo ili baadaye igawanywe.
Kwa zaidi ya miaka miwili wafugaji hao wamegoma kuhama katika shamba hilo la Gawal wakishinikiza kupewa kipaumbele katika kupewa ardhi hiyo, kwa kuwa wao ndio walifukuzwa na serikali ilipochukua ardhi hiyo kuanzisha Shirika la Taifa la Chakula (NAFCO) mwaka 1980.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa