Home » » SERIKALI YASHAMBULIWA KUKITHIRI MIGOGORO YA ARDHI

SERIKALI YASHAMBULIWA KUKITHIRI MIGOGORO YA ARDHI

MBUNGE wa Viti Maalumu, Moza Abeid (CUF), ameishambulia serikali na kueleza kuwa migogoro mingi ya ardhi ambayo inaonekana kupamba moto nchini inachangiwa kwa kiasi kikubwa na serikali.
Moza alisema kuwa serikali inahusika kutokana na kushindwa kuweka kipaumbele katika upimaji wa ardhi, ikiwa ni pamoja na kutokuwa na mipango ya kutoa fidia kwa watu ambao wanatakiwa kuhamishwa kutoka katika maeneo yao.
Mbunge huyo alitoa kauli wakati wa kujadili jinsi ya kutatua migogoro ya mipaka ya Hifadhi ya Taifa ya Tarangire, Pori la Akiba la Mkungunero na vijiji vya jirani.
Akichangia Moza alisema kuwa pamoja na kuwepo kwa baadhi ya watu kudai kuwa migogoro hiyo inasababishwa na wanasiasa lakini tuhuma hizo si sahihi, kwa kuwa chanzo kikubwa ni serikali.
Moza alilazimika kueleza hayo baada ya Mbunge wa Kondoa Kaskazini, Zabein Mhita (CCM), kueleza kuwa wapo baadhi ya wanasiasa ambao wanachochea kuwepo kwa mgogoro wa mipaka hususan katika maeneo ya hifadhi.
Zabein alisema wapo wanasiasa ambao wanakwenda kwa wananchi ambao wapo katika maeneo hayo na kuwachochea kuendelea kufanya shughuli zao za kibinadamu, hatua inayochangia kuwepo kwa machafuko pale wanapoondolewa.
Kauli hiyo ilipingwa vikali na baadhi ya washiriki wa mkutano huo ambapo Moza alidai kuwa madai ya mbunge huyo hayana msingi anayetakiwa kulaumiwa ni serikali kwa kushindwa kutoa kipaumbele kwa ajili ya kupima mipaka.
Mbali na hilo alisema kuwa serikali imekuwa ikijichanganya yenyewe kwa kushindwa kupima mipaka na wakati mwingine kutoa hati ya matumizi ya ardhi kwa wananchi na wakati huo kutoka hati ya kutangaza kuwa ni hifadhi.
Katika mkutano huo wataalamu wengi ambao waliwasilisha mada kuhusu migogoro ya mipaka waliituhumu moja kwa moja serikali kwa kushindwa kutenga fedha kwa ajili ya kupima mipaka.
Naye Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka (CCM), alisema njia pekee ya serikali kuondokana na migogoro ni kutumia busara ya kutenga maeneo ambayo yatawapa fursa wakulima kulima, wafugaji kufuga pamoja na kuweka mipaka sahihi ya hifadhi.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa