Home » » NJIA PANDA;KIZAZI CHA KOMPYUTA NA VIONGOZI NGUMBARU KITEKNOHAMA

NJIA PANDA;KIZAZI CHA KOMPYUTA NA VIONGOZI NGUMBARU KITEKNOHAMA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

KILA mtu anazungumzia au kama hazungumzii yumkini ameshasikia watu au vyombo vya habari vikizungumzia juu ya kompyuta, teknohama au tehama au simuakili, ipod, amazon kindle, na mambo kama hayo. Ila sina uhakika kama wengi wetu tunafahamu ukubwa wa mapinduzi na mabadiiko ambayo yanaashiriwa na uwepo na ujio wa vifaa na zana hizi.
Kwa takwimu zilizopo hivi leo ilhali kampuni ya Simu Tanzania (Tanzania Telecommunication Company Ltd au TTCL ikiwa na simu zake za ofisini na za nyumbani. Simu za kiganjani au simupopote zilianza watu 227,424, walipoingia sokoni kuanzia miaka ya kati ya 1990 sasa wameipaisha idadi ya wamiliki wa simu kufikia zaidi ya milioni 28 na bado inaendelea kukua. Kwa hiyo badiliko kuu la kwanza ambalo liko wazi kwa kila mtu kuona na kusikia ni kwamba zaidi ya nusu ya Watanzania hivi leo wana mawasiiano ya simu kupitia mtandao huu au ule.
Kinachoendelea hivi sasa ni kwa Watanzania wengi kuanza kugura toka kwenye simu za mkononi zisizokuwa na akili kwenda kwenye simu za mkononi zenye akili. Simu ambazo kwa kiasi kikubwa zinaweza kutumika kama vile ni kompyuta ndogo mkononi mwa mtu anayeitumia.
Tangu mwanzo wakati kompyuta zinaingia nchini kulikuwa na wazee waliokuwa wakihofia hata kuzigusa achilia mbali kuzitumia. Jiulize, sasa zinakuja simu za mkononi ambazo zimefanana na kompyuta kwa kiasi kikubwa je, pengo kati ya wanaoona rahisi kuzitumia na wanaoziogopa limekua kiasi gani.
Ninaamini hivi sasa kuna walakini na udhaifu mbalimbali unaotokana na wanaoshika nafasi za uongozi katika serikali, vyama vya siasa, vyuo vikuu na shule, mashirika ya umma na mashirika binafsi kuwa ngumbaru katika matumizi ya teknolojia au teknohama wakati watumishi wa chini ambao wengi wao ni vijana ni stadi wa kutumia kompyuta na simu za mkononi za kisasa.
Kompyuta, simuakili, intaneti na vikorokoro vyake vimezua changamoto mpya katika uendeshaji shughuli za uchumi, jamii, siasa na utamaduni na hata teknolojia yenyewe.
Mtawala au meneja mzuri hivi leo penda usipende lazima pamoja na uweledi na ujuzi wake wa menejimenti awe pia anajua kutumia kompyuta na teknohama kwa mapana na marefu. Teknolojia ya taipuraita ingawa bado iko katika baadhi ya maofisi ya serikali ni teknolojia inayoelekea kwenda kutupa kwenye jalala la takataka baada ya muda siyo mrefu.
Changamoto kubwa na ambayo mimi ninaihofia ni ile itakayoletwa na tofauti ya kasi katika utendaji kazi baina ya vijana na wazee. Vijana watakaokuwa wanataka mambo yao yaende haraka haraka zaidi na wazee ambao kwa hofu yao ya teknohama na teknolojia nyingine zilizopo watataka muda mrefu zaidi katika kuamua na kutekeleza uamuzi uliokwishafanyika.
Kwa upande mwingine wazee watakuwa wakienda kigoigoi na wataendelea kukumbatia ukiritimba, vyeo, ukubwa na ufahari ilhali vijana watapigania kuwepo uwazi, ushindani, uchangiaji na ushirikiano katika nyanja zote za kazi ili kupafanya mahala pa kazi kuwa sehemu inayowatendea haki wananchi wengine wasiopo hapo katika jamii husika. Wazee watang’ang’ania ukirimba na kuwa na woga wa kugawa pato la taifa ili kuleta uwiano katika jamii kwa kasi zaidi kwa kuwa tamaa ya mali, ulimbikizaji na kutokuachia fursa tayari kumeshawalemaza.
Jambo hili litatokea katika kupanga, kutekeleza, kufuatilia na kudhibiti shughuli zinazofanyika katika eneo husika. Mabadiliko haya yanaweza kuzusha mihemuko na misongo baina ya wazee na vijana kutokana na misuguano ya kimawazo, kiuamuzi, kimawasiiano na kiteknolojia.
Kwa sababu hii upo uwezekano mkubwa kwa viongozi kutaka kupunguza kasi ya kuenea na kukua kwa matumizi ya teknolojia mpya kutokana na hofu za kiuongozi na kisiasa na siyo za kiuchumi na kimaendeleo jamii.
Hata hivyo, kitendo cha kuzuia kasi ya kukua na kuenea kwa teknolojia ni kitendo kinachofananishwa na mtu kupambana na ukuta kwani mabadiiko hayazuiliki. Na ni dhahiri katika dunia ya ushindani wale watakaoshindwa kuchangamkia matumizi ya teknoljia fulani watajikuta siku zote wako nyuma ya wale wanaokubali na kuitumia teknolojia mpya haraka zaidi.
Katika kipindi cha mpito inawezekana kuwa na watumishi au rasilimali watu ambayo ni mbumbumbu wa teknohama, lakini katika miezi michache ijayo na wala siyo miaka, watumishi wasiojua teknohama watakuwa ni mzigo kwa wizara, idara, mashirika na taasisi walizomo. Kwa maneno mengine, fumba na kufumbua mtu ambaye atakuwa ngumbaru wa teknoljia muhimu zinazotumika katika shughuli zinazomhusu atakuwa ni sawa na yule mnyama aliyepitwa na wakati na kuzikwa kwenye kaburi la sahahu la teknoljia duniani.
Hii ina maana hakuna tena nafasi kwa wazee kukwepa matumizi ya teknohama na wakiwazuia au kuwakwaza vijana watajikuta wanajikwamisha wenyewe na maendeleo ya taasisi wanazoziongoza.
Ili kuleta kasi katika matumizi ya teknohama ningeliishauri serikali iingie ubia na makamapuni ya ndani na nje ya nchi ili kuwa na madarasa maalumu ya ngumbaru wa teknohama ili tuondoe tofauti kati ya watumishi wanaojua teknohama na wale wasiojua ili kuwatendea Watanzania haki kutokana na yale yanayowezekana kufanyika endapo mtu atakuwa ana weledi na ujuzi wa teknohama katika kazi zake tofauti na yule asiyejua kitu.
Pepe: sammymakilla@hotmail.coom
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa