Home » » Waziri azuia mifugo kuingia mashambani

Waziri azuia mifugo kuingia mashambani

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk Charles Tizeba
WAZIRI wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk Charles Tizeba, amepiga marufuku tabia ya wafugaji wilayani hapa kuingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima nyakati za usiku, kwani jambo hilo linaweza kusababisha mauaji tena wilayani humo.
Tizeba alitoa kauli hiyo juzi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Lupopong’i, Wilaya ya Kiteto, mkoani Manyara ambapo pia alizindua lambo la maji lililojengwa katika kijiji cha Olyapasei.
Lambo hilo limejengwa na serikali na kugharimu zaidi ya Sh milioni 737 na linalenga kuhudumia zaidi ya mifugo 350,000 pamoja na matumizi ya binadamu. Alisema zipo fununu watu wameanza kulisha mifugo usiku kwenye mashamba ya wakulima.
“Suala hilo liachwe litasababisha kuuana tena, Kiteto imekuwa na migogoro ya wakulima na wafugaji, migogoro midogo inayoanzishwa lazima ikemewe,” alisema.
Aliwataka wakulima na wafugaji kupendana na kuepuka mambo yanayohatarisha usalama wao na kuwa kitu kimoja kwa kila mtu kulinda heshima na mali ya mtu mwingine.
“Iwapo kila mmoja ataheshimu mali ya mtu mwingine na kuangalia mipaka ya ardhi aliyotengewa, hakuna migogoro wala mambo yatakayotokea tena,” alisema.
Pia Waziri huyo aliwataka wazee wa kimila kukaa na kuzungumza kuweka hali ya utulivu katika maeneo yao.
Alimtaka mhandisi wa maji atafute mbinu ya kusafisha maji ili kuweza kutumika kwa ajili ya matumizi ya binadamu.
Kuhusu utunzaji wa mazingira aliwataka wakulima na wafugaji kuheshimu vyanzo vya mtiririko wa maji ili waweze kuvuna maji ya kutosha.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk Mary Mashingo, alisema awali wilaya hiyo ilikuwa na malambo 41 lakini kutokana na uharibifu mkubwa wa mazingira, yameharibika na kubaki malambo saba.
Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kiteto, Lailumbe Mollel alisema wafugaji wamekuwa wakihamahama kutokana na kutafuta malisho na maji, hata kusababisha watoto wa wafugaji kukosa masomo.

CHANZO GAZETI LA HABARI LEO


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa