Home » » CHUPA ZA PLASTIKI ZAGEUZWA ‘TOFALI’

CHUPA ZA PLASTIKI ZAGEUZWA ‘TOFALI’

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Imeandikwa na Eric Anthony

Ukuta uliojengwa kwa kutumia chupa
WAKATI chupa tupu za plastiki za maji ya kunywa zikionekana kuwa adui wa mazingira, huku kwa kiasi fulani zikitoa ajira kwa vijana wanaookota na kuziuza kwa kampuni zinazoyeyusha bidhaa hizo, kundi la akinamama nchini limeibuka na ubunifu wa kipekee.

Wanawake hao wanatumia chupa hizo kwa ujenzi wa nyumba imara na za kisasa, badala ya matofali yanayotengenezwa kwa saruji au udongo na kisha kuchomwa kama ilivyozoeleka katika maeneo mengi.
Mapinduzi hayo ya kiteknolojia nchini, yameanza kuonekana katika kijiji cha Msitu wa Tembo, Simanjiro mkoani Manyara ambako kikundi cha wanawake 60 kinachoitwa Sala na Kazi, kimejenga nyumba ya vyumba viwili inayotumika kwa biashara ya duka la kikundi hicho.
Hayo yamethibitishwa na Mwenyekiti wa kikundi hicho, Belsira Samwel aliyezungumza na gazeti hili hivi karibuni na kuthibitisha kuwa ni kweli wamefanikiwa kujenga nyumba kwa kutumia chupa za plastiki, za maji na za soda, zenye ujazo wa lita moja na nusu.
Alisema, mbali ya upatikaji kirahisi wa malighafi hiyo mpya katika ujenzi, inasaidia pia utunzaji wa mazingira. Mathalani, anasema ili kujenga nyumba hiyo ya vyumba viwili, walitumia chupa 4,500 tu, huku ujenzi wote ukigharimu chini ya Sh 300,000 na kwamba gharama kubwa ilikuwa katika kupaua, hasa kwa ununuzi wa mbao na mabati.
“Ni ujenzi wa kisasa, lakini nafuu na unaosaidia uhifadhi wa mazingira,” anasema Mwenyekiti huyo ambaye baada ya kufanikisha ujenzi wa nyumba ya vyumba viwili, aliongeza kuwa, wanakusudia kufyatua majengo zaidi ya miradi, likiwemo la kuhifadhia baiskeli zaidi ya 66 za mradi wa kikundi hicho ambacho huzikodisha kwa wanakijiji wengine.

ZINAVYOGEUZWA ‘TOFALI’
Mwenyekiti huyo alisema wakati wa ujenzi, chupa hizo hujazwa udongo uliochekechwa na kufungwa vizuri, hivyo kutumika kwa ujenzi kwa kutumia udongo na saruji kiasi ili kushikanisha chupa, kama inavyokuwa katika ujenzi wa matofali.
Kwa mujibu wa wataalamu wa aina hiyo ya ujenzi, nyumba huwa imara, zinaweza kuhimili mtikisiko wa ardhi, moto lakini pia wakati mwingine hazipenyezi risasi kirahisi. Mbali ya kutumia chupa hizo katika ujenzi wa nyumba, wabunifu katika nchi mbalimbali wamekwenda mbali zaidi na kutumia chupa hizo kwa ujenzi, hutumika pia kama mapambo ya ndani, hujengea uzio wa nyumba, hutumia kujengea paa mahali pa kuhifadhia magari, hugeuzwa `shamba’ kwa kupanda mimea katika maeneo ya mijini, lakini wapo wanaojenga pia mabanda ya mifugo, kuwekea miswaki, kutengeneza maboti na kadhalika.

KUSAMBAZA TEKNOLOJIA
Anasema wako tayari kusambaza teknolojia hiyo kwa watu au taasisi nyingine, akitolea mfano zipo baadhi ya shule na watu binafsi walioomba kufundishwa teknolojia hiyo ili waweze kuitumia kwa ujenzi wa majengo mapya.
ADUI WA MAZINGIRA
Kwa kiasi kikubwa, chupa za plastiki zinapaswa kutumika tena, lakini sehemu kubwa ya shehena za chupa inaishia kuwa ni taka zinazoendelea kutupwa na hivyo kuhatarisha maisha ya watu wengi duniani.
Inaelezwa kuwa kuna mamilioni ya tani za chupa ambazo ziko ardhini, baharini, kwenye maziwa na mito. Chupa hizi kamwe hazitaoza na zitaendelea kuwa ni sehemu ya kero na uchafuzi wa mazingira.
Hivyo inaonekana kuna haja kwa serikali kuhakikisha zinafanya maboresho ya mitandao ya maji, ili kuhakikisha wananchi wanakuwa na maji safi na salama katika makazi yao.
Katika nchi zilizoendelea zaidi duniani, matumizi ya maji ya chupa za plastiki ni makubwa kutokana na kampeni kubwa zinazofanywa na kampuni zinazozalisha bidhaa ya maji kwa kuwaaminisha kwamba kwa kunywa maji ya chupa wana uhakika wa maisha na usalama wao, ikilinganishwa na maji yanayotoka moja kwa moja kwenye bomba
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa