Home » » SIMANJIRO YAPITISHA BAJETI YA SHILINGI BILIONI 25.3

SIMANJIRO YAPITISHA BAJETI YA SHILINGI BILIONI 25.3

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Mwenyekiti  wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, Jackson Leskar Sipitieck akizungumza kwenye kikao cha Baraza la madiwani wa Halmashauri ya Wilaya hiyo baada ya kupitisha mpango wa bajeti ya shilingi bilioni 25.3 kwa mwaka wa fedha wa 2018/2019 kushoto ni Makamu Mwenyekiti Albert Msole na Katibu Tawala wa Wilaya hiyo Zuwena Omary na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Yefred Myenzi. 
 
MADIWANI wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, wamepitisha rasimu ya mpango wa bajeti ya shilingi bilioni 25.3 kwa mwaka wa fedha wa 2018/2019. 

Akizungumza baada ya kupitishwa kwa bajeti hiyo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Jackson Sipitieck alisema vipaumbele vya bajeti hiyo ni elimu, afya, maji na viwanda. 

Sipitieck alisema suala la kupitishwa kwa bajeti ni jambo moja na utekelezaji ni jambo lingine, hivyo kila mmoja ahakikishe anatimiza wajibu wake ipasavyo wakiwemo madiwani na watumishi, ili kufanikisha hilo. Alisema kila mmoja kwa nafasi yake akisimama kwa nguvu zote, wilaya ya Simanjiro itapiga hatua kubwa ya maendeleo na wananchi wake watakuwa wanapata huduma zao za kijamii kwa ufanisi mkubwa zaidi. 

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Simanjiro, Yefred Myenzi alisema bajeti hiyo ni kwa ajili ya matumizi mbalimbali, ikiwemo miradi ya maendeleo, ruzuku ya uendeshaji ofisi na mishahara. Myenzi alisema wilaya hiyo imeweka mikakati ya kuhakikisha wanaboresha vipaumbele vyao vya elimu, afya, maji na viwanda. Alisema mazao ya mifugo, ikiwemo maziwa, ngozi na nyama inapaswa kuboreshwa ili iwe chachu ya vichocheo vya uchumi. 

Katibu Tawala wa wilaya ya Simanjiro Zuwena Omary aliwapongeza madiwani wa halmashauri hiyo kwa kupitisha mpango huo wa bajeti ya mwaka 2018/2019 kwa manufaa ya wananchi. "Pamoja na hayo tunapaswa kuhakikisha tunatekeleza agizo la kila mkoa kuwa na viwanda 100 kwa sisi Simanjiro kuanzisha viwanda 15 ambayo vitasambazwa kwenye kata zetu na vijiji," alisema Omary. 

Hata hivyo, Diwani wa Kata ya Komolo, Michael Haiyo aliipongeza bajeti hiyo na kusisitiza ikamilishwe kwa vitendo. Haiyo alisema bajeti hiyo imegawanywa bila upendeleo kwani kata zote zimepatiwa miradi ila umuhimu wake utaoneka endapo itatekelezwa kwa vitendo. Diwani wa kata ya Naisinyai, Kilempu Ole Kinoka alisema bajeti hiyo inapaswa kujali suala zima la uboreshaji wa mifugo kwani asilimia kubwa ya wananchi wa eneo hilo ni wafugaji. 

"Sisi kwetu kahawa ya Simanjiro ni mifugo ambayo ni roho ya uchumi, hivyo tunapaswa kulizingatia hilo kwenye utekelezaji wa bajeti yetu," alisema Ole Kinoka.
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa