Home » » Hamashauri Babati yabomoa nyumba za NHC

Hamashauri Babati yabomoa nyumba za NHC



HALMASHAURI ya Mji wa Babati imebomoa nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) zipatazo 52 zilizojengwa katikati ya mji kwa ajili ya kupisha eneo hilo kuwa kituo cha biashara kwa wawekezaji.
Akizungumza wakati wa ubomaji nyumba hizo jana, Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Omary Mkombole, alisema eneo hilo kwa sasa linahitajika  kwa matumizi mengine na pia nyumba hizo zimeshakuwa chakavu, hivyo zinaweza  kuleta madhara kwa wananchi.
“Huu mji kwa sasa unakua na maendeleo yanahitajika zaidi, hivyo basi hatuna budi kuendeleza mji kwa manufaa ya wananchi, na kubomoa nyumba hizi haimaanishi tunawaonea ila ni mpango mkakati wa muda mrefu,” alisema Mkombole.
Alieleza awali walitoa taarifa kwa wamiliki wa nyumba hizo ambao hawakukubaliana na taarifa hizo, hivyo kuamua kupeleka shauri lao Baraza la Nyumba na Makazi wilayani Babati ambako shauri hilo lilitupwa na kupewa siku 90 za kuhama.
Aidha, alisema baada ya siku walizopewa kuisha, wamiliki hao waliomba kuongezewa muda ambapo halmashauri iliwaongezea siku 30.
“Wapangaji waliokuwa wanakaa hapa hatukuwa tukichukua kodi zao na tulisimamisha zoezi hilo tangu mwaka 2010 baada ya kuwatangazia kuhusu kubomoa nyumba hizi na sababu zake,” alifafanua mkurugenzi huyo.
Hata hivyo, alisema halmashauri itatoa viwanja kwa kuwauzia wale wasiopata viwanja na kuongeza kuwa kuna viwanja 20,000 kwa ajili ya makazi.
Wamiliki wa nyumba hizo walidai halmashauri haijawatendea haki, kwani  muda waliopewa kuhama na kupisha eneo hilo ulikuwa mdogo, hivyo wengine kuamua kupanga huku wengine wakikosa mahali pa kuhamia.

Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa