Home » » MJUMITA waomba wataalamu wa misitu

MJUMITA waomba wataalamu wa misitu



WANACHAMA wa Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (MJUMITA) Kata ya Bonga, Wilaya ya Babati, mkoani Manyara, wameiomba serikali kuwapelekea wataalamu wa misitu wakapime msitu wao ili uweze kuingia kwenye orodha ya misitu shirikishi.
Rai hiyo wameitoa jana kwenye mkutano wa kushirikishana juu ya hali ya utawala bora wa misitu iliyowashirikisha wanamtandao hao na wadau wengine wa misitu.
Wanamtandao hao walisema wanahitaji wataalamu wa kupima msitu huo kwa kuwa bado wana changamoto zinazowakabili, ikiwa ni pamoja na migogoro ya mipaka kati ya vijiji na mitaa, motisha kwa walinzi unaosababisha uharibifu mdogo mdogo ndani ya msitu pamoja na kutokuwa na mfuko wa kuendeshea shughuli za msitu huo.
 “Sisi wanamtandao wa Kata ya Bonga tunaomba wataalamu waje wapime msitu ili tuweze kuingia kwenye orodha ya misitu shirikishi jamii/ Tanzania na pia tupatiwe rangi kwa ajili ya kuweka mipaka inayozunguka jamii," walisema wana mtandao hao.
 Aidha, walibainisha kwamba pamoja na changamoto walizonazo, kupitia msitu huo wameweza kupata elimu juu ya kuhifadhi mazingira na kutunza misitu.
Kwa upande wake Mratibu wa (MJUMITA) Kanda ya kati, John Reuben, alisema ili mitandao mingi iweze kufanya vizuri kwenye utunzaji wa misitu na kufanya rasilimali hizo kutumika kwa manufaa ya jamii yote, wanahitaji kupata ushirikiano kutoka kwa viongozi wa vijiji na jamii nzima.
 Reuben alibainisha kwamba lengo la mradi huo ni kuhakikisha kuwa huduma zinazotokana na misitu zinahifadhiwa kwa manufaa ya jamii.

Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa