Home » » Ajali yaua wanne Makatanini

Ajali yaua wanne Makatanini

WATU wanne wamefariki na 32 kujeruhiwa baada ya basi la abiria la Polepole, trekta na bajaji kugongana eneo la Makatanini, wilaya ya Babati mkoa wa Manyara.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mussa Marambo, akizungumza na wanahabari jana kwa niaba ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa Akili Mpwapwa alisema ajali hiyo ilitokea Desemba 7 majira ya saa mbili usiku.
Marambo alieleza chanzo cha ajali hiyo ni trekta kuegeshwa katikati ya barabara bila alama, ndipo basi la abiria lenye namba T 898 BKN aina ya fusso, mali ya Issack Polepole likagongana na trekta aina ya Swaraj lililokuwa halina namba za usajili, huku likiendeshwa na Clement Tuji.
Waliokufa katika ajali hiyo ni Shaibu Olae (25), Mwalimu wa Sekondari Aldersgate Nicodemu Mofuru (27) mkazi wa majengo mapya, Charles Exaud na mwanamke mmoja ambaye hakuweza kufahamika jina lake.
Wakati huohuo waendesha pikipiki wilayani Kiteto maarufu bodaboda wamechoma nyumba ya Mosses Lucas (35) mkulima wa Kibaya wakimtuhumu kwa mauaji ya dereva mwenzao Rasuli Yahaya (17) mkazi wa mafichoni Kijiji cha Mbeli.
Kamanda Marambo alisema tukio hilo limetokea eneo la Ngarenaro Desemba 4 majira ya saa saba mchana.
Alisema Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi kubaini walioshiriki na kusababisha mauaji hayo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa