Home » » Diwani amkana mtendaji kikaoni

Diwani amkana mtendaji kikaoni

DIWANI wa Ganana katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’, mkoani Manyara, Zakayo Tarmo, amemkana mtendaji wake wa kata na kukataa kusomewa taarifa ya maendeleo akimtuhumu hampi ushirikiano katika utendaji ndani ya kata hiyo.
Diwani huyo alitoa shutuma hiyo mbele ya kikao cha baraza la madiwani wakati watendaji wakitoa taarifa za kata zao kwa niaba ya madiwani wao ambapo ilipofika zamu yake alisimama na kutaka taarifa ya kata yake isisomwe kwa kuwa haikuwa sahihi.
Tarmo alieleza mtendaji wa kata yake hakuwa mtendaji bali ni mtawala ambaye anafanya kazi zake bila kutoa ushirikiano kwa diwani wake na kufanya shughuli za maendeleo ya kata hiyo kwa njia anazojua mwenyewe bila kuitisha vikao.
“Huyu mtendaji mliyeniletea ndani ya kata yangu ni mtawala anayeendesha shughuli kibabe na bila kunipa mimi diwani wake ushirikiano wowote, sijui kwa sababu mimi ni CHADEMA, au kwa kuwa mimi si CCM.
“Hiyo taarifa anayotaka kuisoma ameiandaa na nani na ameiandalia wapi mimi sijui, kwa hiyo taarifa hiyo si sahihi na wala siitambui,” alisisitiza Tarmo.
Kwa upande wake mtendaji aliyetuhumiwa, Grace Dofa, hakuweza kuzungumzia shutuma hizo zaidi ya kutoa lawama juu ya diwani wake kwamba anafanya vurugu ndani ya kata hiyo na kusababisha wananchi kumchukia na yeye kufanya chuki juu yake.
Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Felix Mabula, alichukua nafasi yake na kumtaka mtendaji huyo kusoma taarifa aliyoiandaa kwa heshima ya kikao na kutaka suala hilo kuzungumziwa wakati wa majadiliano.
Mabula alibainisha kuwa wanajipanga kufanya uchunguzi wa kina juu ya shutuma hizo ili kubaini mapungufu ya mtendaji huyo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa