Naibu Spika Job Ndugai
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Lemalali
alisema halmashauri yake ililazimika kuwasilisha mashtaka dhidi ya
Ndugai ambaye ni Mbunge wa Kongwa, kwa Waziri Mkuu Pinda wakati
alipotembelea hapa juzi kuwapa pole kufuatia mauaji na
vurugu zilizotokea kati ya wakulima na wafugaji na pia kutafuta ufumbuzi
wa mgogoro huo.
“Ni kweli tumemweleza Waziri Mkuu alipofika hapa kuwa mgogoro huu
unachochewa na Ndugai kwa kutamka hadharani akiwataka wakulima kutoka
nje ya wilaya hii (Kongwa, Kibaigwa) kuja huku kulima kwenye maeneo
ambayo mahakama imepiga marufuku,” alisema.
Alisema Mahakama ya Rufani katika hukumu iliyotolewa mwaka 2012,
iliwapa ushindi halmashauri dhidi ya wakulima 50 matajiri waliokuwa
wakihodhi maeneo makubwa na kuendesha shughuli za kilimo katika Hifadhi
ya Jamii ya Emborei ya Murtangosi, inayomilikiwa na vijiji saba.
“Tatizo langu mimi hapa ni kusimamia hii kesi hadi tumepata ushindi,
ndio naona Ndugai na wenzake wananichukia.
“Suala la kesi ni kweli Ndugai lazima anilaumu mimi, manake
ningelegalega tu wenyeji wanaoishi katika vijiji hivyo wangepata ardhi
kwa malisho ya mifugo yao na kilimo.
“Ndugai anashindwa kusimamia sheria na anachofanya ni uchochezi ambao
hauna misingi,” alisema.
Alisema Ndugai kama Mbunge na Naibu Spika ni mtu mkubwa lakini hata
yeye (Mwenyekiti wa Halmashauri pia ni mtu mkubwa katika eneo la
alilopewa kulisimamia kwa mujibu wa sheria.
“Ndugai amekuwa mtu wa kupamba majukwaa kwa kuhamasisha na
kuchochea mgogoro huu kwa kuwa wengi waliovamia eneo hilo la hifadhi ni
wapiga kura wake kutoka Kongwa hivyo ana maslahi binafsi mgogoro
huu,”alisema na kuongeza wengine wanatoka wilaya mbalimbali za Mkoa wa
Dodoma.
Hata hivyo, alisema watu wanaotaka kuhamia wilayani humo na
kuendesha shughuli za kilimo hawazuiwi alimradi tu wanafuata sheria
kwani Katiba ya nchi inasema kila mtu ana haki ya kuishi po pote pale
mradi tu havunji sheria.
“Sasa hivi hali ya wilaya imekuwa tete kutokana na uchochozi wa
Ndugai, yeye ni kiongozi wa kitaifa anayeshiriki kutunga sheria hivyo
hakupaswa kuhamasisha watu majukwaani,” alisema.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Kiteto, Martha Umbula, alisema anashangazwa
na hatua ya mbunge mwenzake (Ndugai) kumshambulia hadhari na akahoji
uchungu wa mbunge huyo na kama ana maslahi gani katika mgogoro huo.
“Siwalaumu sana kwa sababu wanasiasa tunajuana uwezo wetu, huyu Ndugaiana maslahi gani kwa wilaya ambayo siyo yake.
“Hatujafanya utafiti ni lipi hasa kinachompa msukumo huo, bado ninatafakari na tutazijua sababu hizo hapo baadaye,” alisema.
Ndugai amekuwa akisikika kutoa matamko dhidi ya Mkuu wa Wilaya
Umbula tangu mgogoro kati ya wafugaji na wakulima ulipozuka tena hivi
karibuni akimtaka aachie ngazi wadhifa wake kwa madai ya kushindwa
kuutafutia ufumbuzi.
Amekuwa akifanya hivyo maeneo mbalimbali jimboni kwake Kongwa
katika majukwaa au wakati akishiriki mazishi ya watu waliouawa kwenye
mapigano hayo.
Akizungumzia hali ya amani na utulivu kwa sasa, Umbula alisema
makamishna wawili wa polisi kutoka makao makuu Dar es Salaam wapo
wilayani hapa kuchunguza pamoja na mambo mengine watu wanaotuhumiwa
kufanya mauaji.
Alisema wilaya yake bado inasisitiza agizo la Waziri Mkuu Pinda
alilolitoa juzi katika mkutano wake wa hadhara wilayani hapa ikiwa ni
utekelezaji wa amri ya mahakama ya kuwataka waliovamia hifadhi hiyo
waondoke.
Alisema wilaya itawapatia usafiri wale watakaoshindwa kuhama na
chakula wale ambao vyakula vyao vilichomwa moto katika mapigano hayo.
Chadema yamshauri Rais awafukuze kazi DC na DED
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kutokana na
mgogoro mkubwa wa ardhi kati ya wakulima na wafugaji unaoendelea
wilayani Kiteto ambao umefikia hatua ya kusababisha maafa makubwa ya
umwagikaji wa damu, mauaji ya watu na uharibifu wa mali, Wizara Kivuli,
Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa (TAMISEMI), imemshauri Waziri Mkuu Pinda achukue hatua za
kinidhamu kwa Mkuu wa Wilaya hiyo Martha Umbulla na Mkurugenzi wa
Halmashauri ya Wilaya, Jane Mutagurwa, kisha amshauri Rais Jakaya
Kikwete awafute kazi wote wawili mara moja.
Waziri Kivuli, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), David Silinde,
katika taarifa yake amesema Waziri Mkuu anapaswa kumshauri rais amfukuze
kazi DC Umbulla kwa sababu akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na
Usalama ya Wilaya ya Kiteto, amezembea kuwajibika ipasavyo na
kusababisha kukosekana kwa usalama wa raia na mali zao katika eneo hilo,
hadi kutokea kwa umwagikaji wa damu na mauaji makubwa.
Aidha, Waziri Mkuu Pinda achukue hatua za kinidhamu na kumshauri
Rais Kikwete amfukuze kazi Mkurugenzi wa Wilaya Jane Mutagurwa, ambaye
ndiye mtendaji mkuu wa halmashauri, kwa kushindwa kuwajibika ipasavyo
kuweka mipango bora ya mgawanyo wa ardhi kwa matumizi mbalimbali kwa
wananchi wa eneo husika, hali ambayo ingeweza kuepusha maafa hayo.
Baada ya mahakama kutoa amri ya wananchi hao kuhama, uongozi huo wa
wilaya ulipaswa kuweka mipango ya kusaidia kupatikana ardhi nyingine
kwa ajili ya wananchi hao kuhamia.
CHANZO:
NIPASHE
0 comments:
Post a Comment