Home » » Michuano ya kuboresha Stars yafikia tamati

Michuano ya kuboresha Stars yafikia tamati

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
MASHINDANO ya kusaka nyota wa kuboresha timu ya taifa ‘Taifa Stars’ yanatarajiwa kufikia tamati leo kwa timu mbalimbali kujitupa viwanjani, ambako mkoani hapa, wenyeji Manyara wanawakaribisha Arusha kwenye uwanja wa Babati.
Katika mchezo wa awali uliopigwa jijini Arusha, wenyeji waliibuka na ushindi wa mabao 2-1 kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid.
Mchezo huu unatarajiwa kushuhudiwa na waibua vipaji watano, Peter Mhina, Zamoyoni Mogela, Elly Mzozo na Kenny Mwaisabula ‘Mzazi’ wakiwa chini ya Dan Korosso.
Mbali na mchezo huo, mechi nyingine kundi A itakuwa kati ya Singida na Dodoma, Uwanja wa Namfua na kushuhudiwa na waibua vipaji wanne, Kanali mstaafu Idd Kipingu, Juma Mgunda, Peter Magomba na George Komba.
Kundi B, Mara watawakaribisha Mwanza kwenye Uwanja wa Karume na kushuhudiwa na waibua vipaji watano, Salum Mayanga, Patrick Rweyemamu, Selemani Jabir, Ahmed Simba na Mohamed Ally.
Katika kundi D, Katavi itakuwa wenyeji wa Rukwa kwenye uwanja wa Mpanda na kushuhudiwa na waibua vipaji John Simkoko, Madaraka Bendera, Salvatory Edward, Musa Kisoki na Sunday Manara ‘Computer’.
Kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma itakuwa mwenyeji wa Tabora na kushuhudiwa na waibua vipaji Boniface Pawassa, Edward Hiza, Yusuph Macho na Abdallah Hussein.
Akizungumzia mashindano hayo kwa ujumla, mchezaji wa zamani ambaye pia ni miongoni mwa waibua vipaji, Peter Mhina, alikiri kuwepo kwa vipaji mikoani na kumpongeza Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi kwa kulitambua hilo na kuanza kulifanyia kazi.
“Malinzi kapatia sana kufanya kitu kama hiki, kwani hata sisi tulitokea chini, kwani nakumbuka hata mimi nilikuwa nacheza timu ya taifa wakati nikiwa kidato cha pili, hivyo basi nina imani wachezaji watapatikana, cha muhimu ni sisi wadau kumuunga mkono Malinzi,” alisema Mhina.
Naye Elly Mzozo, mdau na mwalimu wa soka ambaye pia ni Mwenyekiti wa timu ya Friends Rangers, alisema anakumbana na vipaji vingi tangu katika mechi ya kwanza ya Tanga na Kilimanjaro hadi ya Arusha na Manyara.
Mzozo alisema anaumia kuona vipaji kama hivyo haviibuliwi huku timu ya taifa ikifanya vibaya kila kukicha.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa