Home » » HANANG' WAKOSA MAJI SAFI

HANANG' WAKOSA MAJI SAFI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
WANANCHI zaidi ya 3,000 wa Kijiji cha Hedet, Wilaya ya Hanang mkoani Manyara, kwa zaidi ya miaka miwili sasa hawana huduma ya maji safi na salama kutokana na baadhi yao kuvamia na kuondoa stesheni kuu za kusambazia maji zilizokuwepo kwenye njia kuu katika vijiji vya Mara na Getaghul.
Malalamiko hayo yalitolewa na wananchi hao kwa Mbunge wa Hanang, ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk. Mary Nagu kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Hedet.
Walifafanua kuwa pamoja na kuchangia sh. 6,000 kwa kila kaya, lakini wameendelea kunywa maji yasiyo salama huku wakichangia huduma hiyo pamoja na mifugo.
Kwa sasa wananchi hao wanasema wapo tayari kuandamana kuishinikiza serikali kuwapatia maji.
Awali katika taarifa ya Kijiji cha Hedet, iliyosomwa na Ofisa Mtendaji, Bahati Tarimo, walimweleza Waziri Nagu kuwa kijiji hicho hakina huduma ya maji safi na salama tangu Juni 2012, kutokana na wananchi kung’oa stesheni kuu za kusambazia maji katika njia kuu ya kusambazia maji hayo.
Waziri Nagu akijibu malalamiko hayo, alimuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang kuzungumza na wazee wa vijiji vinavyogombea maji.
Pia aliwataka wahakikishe wanaweka utaratibu wa kuchimba visima virefu katika vijiji vya Mara na Getaghul ili kuondoa ugomvi wa maji na kusababisha mabomba kukatwa.
Hata hivyo, katika ziara hiyo ya siku tano wilayani Hanang, Waziri Nagu awali alitembelea na kukagua zahanati inayojengwa, tenki la maji pamoja na sehemu ya kunyweshea mifugo ya vijiji vya Gidagharubu pamoja na kukagua ujenzi wa nyumba za watumishi wa Idara ya Afya zinazojengwa kwa ufadhili wa taasisi ya Mkapa Foundation
Chanzo:Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa