Home » » AUA JIRANI KWA WIVU WA MAPENZI

AUA JIRANI KWA WIVU WA MAPENZI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
WANANCHI wa Kata ya Gisambalang’, Wilaya ya Hanang’, mkoani Manyara bado wanaendelea kugubikwa na wimbi la simanzi na majonzi kutokana na matukio ya mauaji mfululizo yanayotokea katika kata hiyo.
Katika Kitongoji cha Langasesi, Kijiji cha Warang’, usiku wa kuamkia Julai 28, mtu mmoja aliyejulikana kwa jina la Emmanuel Daniel (32), ameuawa kwa kupigwa na jirani yake, Phiri Mampo (33), kwa tuhuma za kutembea na mke wake.
Akizungumzia tukio hilo, Diwani wa kata hiyo, Masalla Bajuta, alisema kwa mujibu wa maelezo ya mtuhumiwa baada ya kumhoji, siku ya tukio Daniel alikuwa amekwenda nyumbani kwa mtuhumiwa ambako alimkuta amelala na kumdai mke wake chakula.
Alisema wakati mwanamke huyo akiandaa chakula, mume wake aliamka na kuwakuta wametoka nje ya nyumba, ndipo alipowafuata na kuanza kumvamia Daniel na kumpigiza ukutani ambapo aliangukia kichwa na kufariki papo hapo.
Diwani huyo alieleza kwamba, baada ya Mampo kuona jirani yake ameshindwa kuamka, alimuangalia na kugundua amefariki, ndipo alimuamrisha mke wake amsaidie kumbeba na kumtupa takribani mita 600 kutoka nyumbani kwao huku wakiwa wamemuwekea ulinzi kama kuna watu watamuona.
Alibainisha kuwa maiti ilishinda eneo hilo hadi Julai 29 majira ya saa 12 jioni, ambapo watoto waliotoka kuchunga waliiona na kukimbia nyumbani kwao kutoa taarifa kwa wazazi wao ambao ni jirani na kwa mtuhumiwa.
Diwani huyo aliongeza kuwa jirani huyo aliyejitambulisha kwa jina la Gitimai aliikuta maiti na kukimbia kwa mwenyekiti wa kitongoji na wakati wanaelekea eneo hilo, mtuhumiwa alishagundua kuwa imeonekana hivyo alichukua jukumu la kuihamisha eneo jingine mbali na mahali hapo. Watu walipofika eneo la awali, hawakukuta maiti zaidi ya damu.
Alisema kuiwa waliamua kupiga yowe na wananachi zaidi walijaa na kabla hawajaanza msako, walikwenda nyumbani kwa mtuhumiwa na kumhoji ila alikataa, lakini wakati huo mke wake alikuwa akilia na kuamua kueleza kilichotokea, ndipo mtuhumiwa alikamatwa na kwenda kuonyesha alipouficha mwili wa marehemu.
Wananchi wa kata hiyo, wamelaani vikali kitendo hicho na wamesema kuwa wameamua kufanya maombi kila mmoja kwa imani yake kumuomba Mungu awaondolee matukio hayo, kwani siku hiyo hiyo mtoto aliyekadiriwa kuwa na miaka mitano alifariki dunia kwa kugongwa na pikipiki na dereva kukimbilia wilaya ya jirani ya Kondoa.
Kamanda wa Polisi mkoani Manyara, Deusdedit Nsimeki, alithibitisha tukio hilo na kusema kuwa marehemu, mtuhumiwa pamoja mwanamke aliyesababisha tukio hilo, wote walikuwa wamelewa.
Kamanda Nsimeki, alisema watuhumiwa wamekamatwa na wako ndani kwa mahojiano na uchunguzi ukikamilika watafikishwa mahakamani.
 Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa