Home » » DAKTARI WA 'KICHINA' ANASWA BABATI

DAKTARI WA 'KICHINA' ANASWA BABATI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
WATU saba wametiwa mbaroni na Jeshi la Polisi mkoani Manyara, akiwemo daktari bandia na wengine katika mtandao wa wizi wa magari uliyotokea jijini Dar es Salaam kwa nyakati tofauti.
Kamanda wa Polisi mkoani Manyara, Deusdedit Nsimeki, alisema wamemtia mbaroni Godlone Sozigwa (27), mkazi wa Dar es Salaam ambaye alijifanya daktari katika hospitali ya mkoa akiwa amepeleka maombi ya kufanya kazi kwa muda.
Nsimeki, alieleza kwamba Sozigwa alikuwa na vyeti mbalimbali vya kughushi ambavyo vilionyesha amehitimu elimu ya udaktari chuo cha Muhimbili huku akiwa na mavazi rasmi ya udaktari.
Alibainisha kwamba mtuhumiwa alikamatwa kupitia wasiri wa jeshi hilo pamoja na kushindwa kujibu maswali kadhaa ya kitaaluma wakati akihojiwa baada ya kupokelewa maombi yake.
Akizungumza mbele ya waandishi wa habari, Sozigwa alikiri kughushi vyeti na kuomba kazi kutokana na hali ngumu ya maisha inayomkabili, huku akidai alisomea taaluma hiyo katika kampuni moja ya Kichina ambayo alikuwa akifanya kazi jijini Dar es Salaam.
Alisema alisomea taaluma hiyo kwa miaka minne na aliona anao uwezo wa kuhudumia wagonjwa kama madaktari wengine, hivyo akaona ili kujikimu kimaisha atume maombi katika hospitali hiyo ambayo alidai aliambiwa kuna uhaba wa madaktari.
“Nikweli hivi vyeti nimefoji, lakini mimi na wenzangu tulisomea udaktari kwa muda wa miaka minne katika kampuni moja ya kichina ambako tulikuwa tukifanya kazi na kilichonifanya kufanya hivyo ni ugumu wa maisha unaonikabili,” alieleza mtuhumiwa huyo.
Aidha, Kamanda Nsimeki, alisema watuhumiwa watano waliohusika kwenye wizi wa gari aina ya Canter Toyota lenye namba T 233 CMR eneo la Mbagala kwa kuvushwa kwenye uzio, wamerudishwa jijini Dar es Salaam baada ya uchunguzi kukamilika.
Aliwataja kuwa ni Said Salum (36), ambaye ndiye alikutwa na gari hilo na Albert Philipo (46), wakazi wa Negamsi mjini Babati, Hamad Ally (32), mkazi wa Maisaka mjini Babati, Hamisi Juma (48), na Hashim Hassan (49), wakazi wa mkoani Arusha.
Kamanda alimtaja mtuhumiwa mwingine kuwa ni Rajab Marobo (42), ambaye anahusishwa na wizi wa gari aina ya Spacio yenye namba T 498 CCC iliyoibiwa Tabata Dar es Salaam ikiwa kwenye maegesho, ambako imedaiwa dereva wa gari hilo alipanga njama na mlinzi.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa