Home » » HALMASHAURI YAKUSANYA ASILIMIA 94 YA MAPATO

HALMASHAURI YAKUSANYA ASILIMIA 94 YA MAPATO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

HALMASHAURI ya Wilaya ya Babati vijijini mkoani Manyara kwa kipindi cha mwezi Juni 2013 hadi Juni 2014 imekusanya jumla ya sh.1,758,784,299 kutokana na mapato yake ya ndani ambayo ni sawa na asilimia 94 ya makisio ya mwaka ambayo yalikuwa sh. 1,867,801,000.

Hayo yalisemwa juzi na Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati, Bw. Dominic Kweka, wakati akisoma taarifa ya Halmashauri, kwenye kikao cha Baraza la Madiwani cha kufunga mwaka wa fedha kilichohudhuriwa na wakuu wa idara pamoja na wananchi katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri.

Akisoma taarifa hiyo ya halmashauri yao kufanya vizuri katika makusanyo ya ndani, Bw. Kweka alisema, ukusanyaji mzuri wa mapato ya ndani umewawezesha kupata hati safi na kutaka juhudi hizo ziendelee ili kuiweka halmashauri pazuri kimaendeleo.

 

Naye kwa upande Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Bw. Nicodemas Tarmo akifungua kikao hicho aliwataka watumishi kuzingatia kanuni za utendajikazi kwa kufanya kazi kwa uadilifu na kuepuka tabia za utoro na ulevi saa za kazi.

Bw.Tarmo alisema, "watoro na walevi kazini wasilelewe kwa kutafuta visingizio bali wachukuliwe hatua za kinidhamu na siyo kuwahamisha na kuwapeleka maeneo mengine na kwenda kuambukiza matatizo kwa wengine, hasa walevi ni bora tubaki na wanywaji lakini siyo walevi."

Pia Bw. Tarmo aliwahimiza madiwani katika kata zao kufanya kazi ya ziada ya kuwashawishi wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya wa Jamii (CHF) ili kuboresha huduma ya afya vijijini kwani inaonesha kwamba ujumbe huo bado haujawafikia wananchi walio wengi.

Kwa upande wa migogoro ya ardhi iliyokithiri katika halmashauri hiyo, Bw Tarmo aliwataka madiwani waelimishe jamii kupitia mikutano itakayokemea vyanzo vya migogoro na kuzuia uuzaji holela wa ardhi unaofanyika mitaani bila kushirikishwa halmashauri za vijiji kwani ndiyo wenye dhamana ya ardhi kijijini.

Aidha katika kikao hicho, mambo yaliyojadiliwa ni pamoja na ukosefu wa chakula cha mchana kwa shule za msingi, ambapo Diwani wa kata ya Bashnet, Bw. Laurent Tara aliposema kwamba inashangaza kuona wito huo wa kuchangia chakula cha mchana kwa watoto wa shule za msingi unakuwa mgumu ilhali wananchi haohao wanakubali kuchangia chakula kwa wanafunzi wa shule za sekondari.

Akichangia hoja hiyo Bw. Tara alisema, "kwa nini wazazi wanashindwa kuwahurumia hawa watoto wadogo wa shule za msingi kwa kuwachangia chakula cha mchana na badala yake wanakubali kuwachangia wale wakubwa walioko sekondari, mbona huu ni ukatili tuchukue hatua za kumaliza tatizo hili.”

Chanzo:Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa