Home » » TULIPOFIKIA TUSIRUHUSU TENA SIASA IENDESHE UCHUMI

TULIPOFIKIA TUSIRUHUSU TENA SIASA IENDESHE UCHUMI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Katika utawala wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa na uchumi huria, kuendeleza mfumo uleule wa kizamani katika medani ya siasa, mathalan, dhana ya “chama tawala”; “chama kushika hatamu za uongozi”; “chama kimoja”; “zidumu fikra za mwenyekiti”, kwa moyo wa dhati kabisa, lazima niseme kwamba, kwa mtindo huo, Watanzania tutajikaanga kwa mafuta yetu wenyewe.
Mabadiliko au mageuzi ya kiuchumi tuliyoyatarajia hayatakuwepo asilani . Nchi za wenzetu duniani, na hata za majirani zetu, zitasonga mbele kiuchumi, tena kwa kasi, lakini sisi tutabakia hapa tulipo, na pengine tukarudi nyuma zaidi kimaendeleo.
Kwa sababu, sisi tutakaposinzia, tutawapa mwanya wenzetu wa nje waje zaidi kuwekeza nchini. Wachote zaidi kilichopatikana, na kukipeleka kwao, wakituacha na umaskini wetu.
Tumekiona hicho kikifanyika katika sekta ya madini na rasilimali nyingine za nchi, ambazo Watanzania wenyewe hawakuwa na ubavu wa kuwekeza vilivyo.
Ukweli ni kwamba Watanzania tutaendelea kujikongoja kwa mwendo wa Konokono, tukiomba Mungu tusipishane na gari yanayoendeshwa na wawekezaji kutoka nje wenye mitaji mikubwa’.
Watanzania tutabakia tumenasa, na hata ikibidi kuzama zaidi katika lindi la ufukara na umaskini .
Watu hawatakuwa na uwezo wa kuwekeza na kuendesha miradi mikubwa ya kiuchumi yenye uwezo wa kuleta mabadiliko makubwa haraka (BRN), kama wengi walivyotarajia.
Kwa nini ? Kwa sababu tutakuwa tumekubali kuruhusu ushindani katika uchumi, yaani nguvu za soko na sekta binafsi ziongoze uchumi na biashara.
Lakini, bado tutakuwa wagumu au tumeshikwa na kigugumizi katika kuruhusu ushindani wa kweli katika medani ya siasa kwa kuruhusu au kukubali kuwa na Katiba mpya itakayoruhusu na kufungua milango ya ushindani wa kisiasa, na Katiba hiyo mpya kuwa mhimili wa kweli wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa, kwa kutengeneza uwanja ulio sawa wa ushindani wa kisiasa, miongoni mwa vyama vya siasa nchini, bila kuruhusu ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka.
Wenzetu wamepiga hatua kubwa kiuchumi kwa sababu ya ubora na umakini wa katiba zao. Katiba zao zimejenga ushindani wa kisiasa uliokidhi mahitaji ya ushindani wa kiuchumi .
Kwa kuwa tumekubali ushindani wa kiuchumi, hatuna budi kukubali ushindani wa kweli na wa haki kisiasa. Vitu hivyo viwili daima huenda pamoja, vikiachana lazima patatokea mtafaruku kimaendeleo.
Ziko wapi tena nguvu za umma katika vyama vya siasa, wakati mashirika yao ya umma yaliuawa na wajanja wachache na wao wakaachwa yatima ?
Ziko wapi tena zama za nguvu ya umma, kwa kutoa ahadi za nafasi nyingi zaidi za ajira, na hali bora zaidi ya maisha, wakati viwanda vyao vilipukutika na kubakia maghofu na nchi kugeuzwa dampo la bidhaa duni kutoka nje?
Wakati migodi yote muhimu ikimilikishwa kwa wageni (kampuni za kimataifa), na wao wakibakia na vumbi lisilo na utajiri wa uhakika?
Katika mazingira kama hayo ya uchumi shindani, bila ya kuruhusu siasa shindani itakayoongoza na kulindwa na Katiba mpya na bora, iliyobeba maudhui hayo ya mageuzi ya kiuchumi, basi tujue kwa hakika kwamba Watanzania tutajikaanga kwa mafuta yetu wenyewe.
Hakuna cha maana kitakachofanyika kiuchumi katika dunia hii ya utandawazi. Utegemezi wa kiuchumi na kiteknolojia utazidi kuongezeka kwa kukosa ubunifu wa kifikra na mawazo mbadala.
Tony Adams ni mchambuzi wa masuala ya uchumi anapatikana kupitia barua pepe: majaliwa.adamms@gmail.com.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa