Home » » CWT NGORONGORO WAMLALAMIKIA MKURUGENZI

CWT NGORONGORO WAMLALAMIKIA MKURUGENZI

CHAMA Cha Walimu Nchini (CWT), wilayani Ngorongoro kimemlalamikia Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, John Mgalula kwa kukataa kuunda Baraza la Wafanyakazi.
Imedaiwa kuwa hali hiyo imepunguza ari ya watumishi wa halmashauri kufanya kazi hasa walimu jambo linalochangia shule za wilaya hiyo kufanya vibaya kitaaluma.
Hayo yalisemwa juzi na Katibu wa CWT wilayani hapa, Emanuel Ledio alipozungumza na Tanzania Daima kuhusu kero ya muda mrefu.
Alisema CWT ilimuandikia barua mara mbili, wamekutana na mkurugenzi huyo ofisini kwake mara mbili wakimuhimizi kuunda chombo hicho kisheria lakini amegoma.
“Hilo ndiyo jukwaa pekee la wafanyakazi kueleza dukuduku zao ili kuboresha utendaji kazi, hapa mnaweza kutengeneza mkataba wa hali bora kazini lakini mkurugenzi huyu hataki kuunda na haelezi sababu za yeye kutounda baraza hilo,” alisema Ledio.
Alitaja kero wanazokumbana nazo walimu wa Ngorongoro kuwa ni kwenda kilomita 200 kufuata mishahara yao wilayani Karatu na wakati mwingine hulazimika kulala huko kutokana na shida ya usafiri.
Akizungumzia suala hilo kwa njia ya simu, Mgalula alikana kupata barua na kukutana nao kuhusu jambo hilo hivyo aliwataka wafike ofisini kwake.
“Wamekuja kulalamika kwako mbali kiasi hicho? Kwa nini wasije ofisini kwangu tuongee uso kwa uso? Sasa kwa kuwa wameamua kukufuata basi waambie waje ofisini kwangu Jumatatu asubuhi na wajitambulishe kuwa wao ndio waliokuja kwenye ofisi za magazeti tutayazungumza na hilo baraza tutaliunda,” alisema mkurugenzi huyo.
 chanzo;Tanzania Daima
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa