Home » » MATUKIO YA ELIMU YA KUKUMBUKWA 2014

MATUKIO YA ELIMU YA KUKUMBUKWA 2014

Matukio kadhaa yanaufanya mwaka 2014 kuwa wenye kumbukumbu ya aina yake katika sekta ya elimu nchini. Fuatana na mwandishi kujua matukio hayo ya kielimu yaliyoteka hisia za watu wengi kwa mwaka mzima.
Mfumo mpya wa madaraja ya ufaulu waibua mjadala
Februari 22, mwaka huu, Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), limetangaza Matokeo ya Mtihani wa Taifa wa kidato cha nne wa 2013, huku ufaulu ukiongezeka kwa asilimia 15.17 kupitia mfumo mpya wa upangaji ambao ulipanua wigo wa alama na madaraja ya ufaulu.
Upangaji wa alama hizo ni A: 75-100, B+:60-74, B:50-59, C:40-49, D:30-39, E:20-29 na F:0-19. Kabla ya mabadiliko hayo, alama zilizokuwa zikitumiwa kupanga matokeo ya kidato cha nne zilikuwa ni A:80-100, B:65-79, C:50-64, D:35-49 na F: 0-34.
Hata hivyo, wadau wengi wa elimu waliokosoa mfumo huo akiwamo Profesa Kitila Mkumbo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,a aliyesema mabadiliko hayo yalilenga kuongeza ufaulu ili kuridhisha wapiga kura kupitia mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Shule 10 bora 2013 zaporomoka
Julai 17, mwaka huu shule za sekondari zilizokuwa kwenye orodha ya 10 bora katika matokeo ya kidato cha sita mwaka 2013, zimeporomoka na shule isiyo maarufu ya Igowole kutoka mkoani Iringa ilichomoza kutoka nafasi ya nane hadi ya kwanza mwaka huu.
Aliyekuwa kaimu katibu mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Dk Charles Msonde alisema katika matokeo ya mwaka jana, kati ya shule 10 zilizokuwa na watahiniwa zaidi ya 30, ni shule nne pekee zimeendelea kuwamo katika kundi la shule 10 bora kitaifa mwaka huu.
Shule zilizoporomoka mwaka huu ni Marian Girls (Pwani) iliyokuwa ya sita mwaka huu wakati mwaka 2013 ilishika nafasi ya kwanza. Shule zilizotoka patupu katika orodha hiyo mwaka huu ni Mzumbe (Morogoro) iliyokuwa ya pili, Ilboru Arusha (ya nne) na Mtakatifu Mary Mazinde Juu ya Tanga (ya sita).
Wizara yaifuta EMAC
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ilisikia kilio cha muda mrefu cha wadau wa elimu kuhusu kuwapo kwa vitabu visivyo kuwa na viwango vilivyokuwa vikipewa ithibati na iliyokuwa Kamati ya Kusimamia Vifaa vya Elimu (EMAC).
Septemba mosi, wizara ikaifuta kamati hiyo na kuhamishia majukumu yake kwa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET)
Kwa mujibu wa ufafanuzi uliotolewa na wizara hiyo, TET kwa sasa itakuwa na mamlaka ya kuchapisha vitabu na kuvisambaza kwa utaratibu wa kitabu kimoja kwa kila darasa na kila somo kuanzia ngazi ya awali, msingi, sekondari na vyuo vikuu.
Uamuzi wa kuifuta EMAC hasa baada mjadala mzito wa kitaifa kuhusu ubora wa vitabu ulioibuliwa na Mbunge wa kuteuliwa, James Mbatia ambaye Julai akiwa bungeni alisema vitabu vingi vina maarifa yanayowapotosha wanafunzi.
Nusu wafaulu darasa la saba
Novemba 6, wazazi wengi walipata faraja baada ya Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), kutangaza matokeo ya mtihani wa darasa la saba mwaka 2014, yakionyesha kuwa zaidi ya nusu ya wanafunzi waliofanya mtihani huo Septemba mwaka huu, walifaulu.
Matokeo hayo yaliyotangazwa na Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde, yalionyesha kuwa ufaulu uliongezeka kwa asilimia 6.38 ikilinganishwa na mwaka 2013. Shule ya Twibhoki iliyopo mkoani Mara ndiyo iliyoibuka kinara kitaifa kati ya shule 15,867 ikifuatiwa na shule za Mugini, Peace Land na Alliance zote za mkoani Mwanza.
Hata hivyo, wadau walikosoa matokeo hayo wakisema miongoni mwa waliofaulu wapo wanaoshindwa stadi za msingi za kusoma na kuandika.
Tanzania yang’ara kusini mwa Afrika
Wakati wananchi wakiendelea kutafakari kinachoendelea juu ya udhaifu wa elimu nchini, Desemba 9, mwaka huu Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (Unesco) kupitia ripoti yake ya Elimu kwa Wote (EFA), lilitoa matokeo ya kushangaza.
Ofisa mipango na mwakilishi wa Unesco nchini, Zulmira Rodrigues, alisema tangu kuwekwa kwa malengo sita ya elimu kwa wote mwaka 2000, Tanzania ilishavuka lengo la asilimia 57.1 kwa kupata asilimia 72.2.
Kwa mujibu wa EFA, lengo la sita ni kushughulikia changamoto ya kujua kusoma na kuandika.
Necta yatangaza mfumo mpya
Tukio lililofunga mwaka lilijiri Desemba 13, mwaka huu baada ya Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), kuanzisha mfumo mpya wa kupanga matokeo ya kidato cha nne mwaka huu na ya kidato cha sita mwakani, ambapo kwa sasa madaraja yatapangwa kwa wastani wa pointi (GPA) badala ya jumla ya pointiMsonde alisema hayo katika mkutano wa wadau wa kampeni ya elimu kwa watoto wa kike uliofanyika mkoani Dodoma. Alisema mfumo huo siyo mpya kutumiwa na Necta kwa sababu umekuwa ukitumiwa katika kupanga matokeo ya wanafunzi wa vyuo vya walimu. Alisema kuwa thamani ya madaraja itabaki kuwa ilivyo ila kutakuwa na mfumo unaolingana na upangaji matokeo kama ilivyo katika vyuo vya ualimu. Lengo la mfumo huo aliongeza kuwa ni kuwezesha kuwa na mfumo unaofanana katika ngazi zote za elimu nchini.
Chanzo:Mwananchi

 Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa