Home » » TNBC yaagiza Baraza la Biashara mkoani Manyara kufanya kazi zaidi

TNBC yaagiza Baraza la Biashara mkoani Manyara kufanya kazi zaidi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

KATIBU Mtendaji wa Baraza la Biashara la Taifa la Biashara (TNBC), Raymond Mbilinyi, ameshauri Mkoa wa Manyara kufanya kazi kwa bidii na kuongeza ushirikiano miongoni mwao ili kuzidi kusaidia kujenga mazingira bora ya biashara na uwekezaji mkoani humo kwa maendeleo ya mkoa na nchi nzima kwa ujumla.

Mbilinyi alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari mkoani humo mwishoni mwa wiki. Alisema wajumbe hawana budi kuhakikisha wanafanya kazi kwa ushirikiano zaidi ili kukuza shughuli za biashara na uchumi.
"Napongeza baraza hili ambalo limejumuisha wajumbe kutoka sekta ya umma na binafisi kwa kuonesha mwamko mkubwa wa kufanya kazi," alisema.
Alisema biashara na uwekezaji katika mazingira ya sasa unategemea ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi kukaa pamoja na kujadili namna ya kuendeleza biashara na uwekezaji.
Alisema wajumbe wa baraza wanatakiwa kujadili kwa uwazi vikwazo na njia ya kuyatatua na pale inaposhindikana yatasababisha kupatiwa suluhisho katika ngazi ya taifa.
Alisema Desemba mwaka 2013 ulifanyika mkutano wa saba wa Baraza la Biashara la Taifa, chini ya Uwenyekiti wa Rais Jakaya Kikwete na ajenda zilikuwa tatu ikiwemo Watanzania kushiriki katika uchumi, Matokeo Makubwa Sasa na kuboresha mazingira ya biashara.
Alisema ajenda hizo zinatakiwa kufanyiwa kazi katika ngazi ya mkoa ili kupata ufanisi zaidi.
"Nitafurahi kuona baraza la mkoa huu mkiendeleza hili kwa nguvu ili kufikia malengo yanayokusudiwa," alisisitiza Mbilinyi. Akifafanua zaidi alisema ngazi ya mkoa na wilaya zikiweka mazingira bora ya biashara itasaidia wafanyabiashara kushiriki vema na kuwa hayo yote yanategemea zaidi wajumbe hao wa baraza.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Biashara la Mkoa wa Manyara, ambaye pia Mkuu wa Mkoa huo, Elaston Mbwilo, alisema sekta ya umma itahakikisha inashirikiana vizuri na sekta binafsi kupitia baraza hilo.
"Sekta ya umma itafanya kazi kulingana na jinsi tunavyojadili hapa katika kukuza biashara na uwekezaji," alisema Bw. Mbwilo. Alisema mkutano huo ulikuwa ni fursa kubwa kwao kuzungumzia masuala yanayolenga kujenga biashara na uwekezaji wa mkoa wao.
Pia alitoa mwito kwa baraza hilo kuziunganisha sekta ndogo za ufugaji na kilimo ambazo ndizo shughuli kuu za mkoa huo, lakini zimekuwa hazina uhusiano mzuri. Aliagiza kufanyika kongamano ambalo litawaunganisha wafugaji kwa kuwa hawana umoja kama ilivyo kwa wakulima.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa