Home » » Vijiji 20 kunufaika mradi wa maji Mbulu

Vijiji 20 kunufaika mradi wa maji Mbulu

JUMLA ya vijiji vipatavyo 20 vya Wilaya ya Mbulu Mkoa wa Manyara, ambavyo vilikuwa vikikabiliwa na tatizo la uhaba wa maji, vinatarajia kunufaika na huduma hiyo baada ya kuwekwa kwenye mpango wa mradi kumaliza tatizo hilo.

Hayo yamebainishwa juzi na Mhandisi wa maji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Bw. Ramadhan Mulungu, kwenye baraza la madiwani, ambapo alisema kuwa vijiji 20 vinatarajia kupata huduma hiyo mwezi Julai mwaka huu, na hivyo wananchi kuondokana na tatizo hilo la maji.
Bw. Mulungu alisema vijiji hivyo 20 vitakavyonufaika na huduma hiyo ya maji vipo kwenye kata za Geterer, Endamilay, Masqaroda, Gunyoda, Tumati, Muday, Masieda, Maghang, Maretaduna Endagaw.
Alisema, serikali kupitia wizara ya maji imeweka mpango wa miaka mitano wa kuhakikisha matatizo ya maji yanakwisha kupitia mpango wa awamu ya pili wa upatikanaji wa maji vijijini kwa kutenga vijiji 20 kwa kila wilaya kupata maji.
"Kupitia fursa hiyo ya kila vijiji 20 kwenye wilaya zote nchini kupata maji, wananchi wa Wilaya ya Mbulu ambao walikuwa wanakabiliwa na tatizo hilo au kufuata maji umbali mrefu watapata huduma hiyo," alisema Bw. Mulungu.
Hata hivyo, Naye Diwani wa kata ya Daudi, Bw.Paul Sulle aliwataka watumishi wa idara ya maji wilayani humo ,kufanya tafiti na kutoa uzito kwenye maeneo yanayopatikana maji, hivyo kunufaisha idadi kubwa ya watu.
"Tatizo la maji lipo, hivyo kutokana na hali ilivyo hivi sasa inatakiwa mfanye utafiti kwanza kabla ya kufanikisha mpango huo, kwani kuna baadhi ya maeneo kuna maji ya kuchota hivyo mkitoa kipaumbele wengi watanufaika na huduma hiyo," alisema Bw.Sulle.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa