Home » » SERIKALI IBORESHE VITENDEA KAZI SHULENI

SERIKALI IBORESHE VITENDEA KAZI SHULENI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
KUSHUKA kwa kiwango cha elimu nchini kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na upungufu wa baadhi ya vitendea kazi shuleni pamoja ari ya ufundishaji ya walimu kupungua kutokana na mishahara midogo wanayolipwa.
Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa jana na Mkuu wa Shule ya Sekondari Wakisimiri, Emmanuel Kisongo, kwenye mkutano wa Kanda ya Kaskazini Magharibi ulioshirikisha mikoa ya Arusha na Manyara.
Kisongo ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wakuu wa Shule za Sekondari (Tahossa), alisema ili kufanikisha malengo ya mpango wa serikali wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) kwa upande wa sekta ya elimu, serikali inatakiwa kuboresha maeneo  hayo.
“Matokeo makubwa sasa hayawezi kuja hivi hivi, yanatakiwa yaandaliwe. Shule zinafanana, lakini changamoto zake zinatofautiana, hasa katika suala la miundombinu ya ufundishaji, hivyo serikali inatakiwa kuangalia pale penye mapungufu paboreshwe,” alisema Kisongo.
Alitoa wito kwa serikali kuangalia suala la siasa shuleni na kusema kuna baadhi ya wanasiasa, hasa madiwani wamekuwa na tabia ya kuingilia taratibu za shule hadi kukwaruzana na walimu kwa maslahi yao binafsi.
“Ninaweza kusema siasa imebeba kila kitu katika jamii zetu kwani kuna wakati wanasiasa hao, hasa madiwani wamekuwa wakiingilia kazi za walimu kwa lengo la kulinda wapiga kura wao, wanatumia shule kama jukwaa la siasa na sio sehemu ya kutolea taaluma,” alisisitiza.
Awali akifungua mkutano huo, Mkuu wa Wilaya ya Babati, Khalid Mandia, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Elaston Mbwilo, aliwataka wakuu hao wa shule kutowakatisha tamaa walimu wageni wanaopangiwa kufundisha katika shule zao, na badala yake kuwatia moyo ili waweze kufanya kazi zao kwa ari na kufanikisha azma ya Matokeo Makubwa Sasa.
 Chanzo:Tanzania 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa