Home » » HOT NEWS: MGOGORO WAIBUKA JUU YA NANI MMILIKI WA TIMU YA TANZANITE MANYARA?

HOT NEWS: MGOGORO WAIBUKA JUU YA NANI MMILIKI WA TIMU YA TANZANITE MANYARA?

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Na Bertha Mollel – Manyara

Mgogoro mkubwa umeibuka juu ya nani mmiliki halali wa timu ya Tanzanite FC ambao ni mabingwa wa mkoa wa manyara,  baada ya wadau wa kandanda katika mji mdogo wa mererani kuvutana na mfanya biashara mdogo wa madini ya tanzanite Charles Andrew “Mnyalu”  anayeihudumia timu hiyo kwa sasa.

Hali hiyo imejitokeza baada ya Tanzanite  kufanya vibaya katika ligi ya mabingwa wa mikoa iliyomalizika hivi karibuni ambapo  Tanzanite waliondolewa katika ligi hiyo kutokana na  wachezaji wake  kumdunda mwamuzi na baadaye kushindwa kulipa faini waliyopangiwa hali iliyosababisha Tanzanite FC kuenguliwa katika ligi hiyo.

Wadau hao kutoka mirerani wamemshutumu Mnyalu kuimiliki timu kinyume na makubaliano ya kuitafutia wafadhili na badala yake kujitangaza kuwa ni mmiliki wa timu hiyo baada ya kukabidhiwa leseni na cheti cha usajili wa timu.

Walisema kuwa kutokana na kujitangaza huko  Mnyalu amekuwa akipata misaada mbalimbali na kujinufaisha  kwa misaada hiyo anayopata kwa mwamvuli wa kuwa mmiliki wa Tanzanite FC wakati si kweli bali alikuwa kama mfadhili tu.

Kocha wa timu hiyo, Ally Matimbwa anayesimama kwa niaba ya viongozi halali wa Tanzanite FC amesema yeye ndiye mmliki halali wa Tanzanite na kosa kubwa walilolifanya ni kumkabidhi Mnyalu timu na baadaye kuwageuka na kuihodhi timu hiyo moja kwa moja.

“Sisi ndie wamiliki halali wa timu ya Tanzanite FC na tulikuwa tunashindwa kumudu baadhi ya gharama ambapo tuliamua kutafuta wafadhili na kumpata Mnyalu ambapo kosa kubwa tulilofanya ni baadae kumuamini sana na kumpatia document za timu hali ambayo sasa anatamba kuwa timu ni yake”

Akizungumzia mgogoro huo mmiliki wa sasa wa Tanzanite FC,  Charles Andrew “mnyalu”  akionyesha kushangazwa na tuhuma hizo alisema kuwa kuna baadhi ya watu wanatumika kumchafua baada ya kuona maendeleo ya timu ya Tanzanite kutoka wilayani hadi sasa inatisha katika ngazi ya taifa.

“Hizo ni kelele tu za watu kwa lengo la kunichafua baada ya kuona timu inapaa angani kutoka wilaya, mkoa na sasa taifa,  ndio maana kelele nyingi zinaibuka ila kama ujuavyo dua la kuku haliwezi kumpata mwewe ndivyo hivyo na mimi wala kelele hizo hazitanirudisha nyuma kuihudumia timu hiyo na nazidi kusema kwa herufi kubwa kuwa mimi ndie mmiliki halali wa timu na anaepinga ajitokeze” Alijitamba Mnyalu.

Hata hivyo jitihada za Tanzania daima kutaka kujua juu ya nani hasa mmiliki wa timu ya Tanzanite FC ulifika hadi chama cha soka wilayani simanjiro (SIDFA) ambapo nao walithibitisha kuwa Charles Andrew “mnyalu” ndiye mmiliki halali wa timu hiyo.

Akizungumza na Tanzania daima, Katibu wa SIDFA, Zefania Simon alisema kuwa  Mnyalu ndie mwenye vyeti vya usajili na amekuwa akiihudumia timu hiyo tangu ligi ya wilaya,mkoa na sasa ligi ya mabingwa wa wilaya ambapo ameshangazwa na hali ya baadhi ya watu kujitangaza kuwa wao ndio walikuwa wamiliki wa timu ya Tanzanite FC.

Kufuatia madai hayo, Zefania  ametoa onyo kali kwa watu hao wanaojiita wamiliki wa timu ya Tanzanite FC  na kuwataka kufuata taratibu halali kwa mujibu wa katiba ya chama juu ya uhalali huo.

Alisema kuwa watu hao hadi sasa  wakiitwa kwenye vikao na mikutano ya SIDFA wamekuwa hawajitokezi na badala yake kulaumu na kutoa shutuma za kunyang’anywa timu nje ya vikao halali hali ambayo ni kinyume na sheria na taratibu za soka.

Uongozi wa chama cha soka mkoani  Manyara (MARFA) kupitia mwakilishi wa vilabu Fortunatus Kalewa umetoa tamko kuwa hawawezi kuzungumzia umiliki wa timu hiyo kwani wao hawana timu bali timu ni za wilaya hivyo tamko litakalotolewa na wilaya ya simanjiro ndio tamko halali na tayari wilaya ya simanjiro imeidhinisha kuwa timu ya Tanzanite FC ni mali halali ya Charles Andrew  “mnyalu”

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa