Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MGOGORO umeibuka juu ya umiliki halali wa timu ya Tanzanite FC
ambayo ni mabingwa wa Mkoa wa Manyara, baada ya wadau wa soka katika
mji mdogo wa Mirerani kuvutana na mfanyabiashara mdogo wa madini ya
tanzanite, Charles Andrew ‘Mnyalu’ anayeihudumia kwa sasa.
Hali hiyo, imejitokeza baada ya Tanzanite FC kufanya vibaya katika
Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL), iliyomalizika hivi karibuni, ambapo
iliondolewa baada ya wachezaji wake kumdunda mwamuzi na baadaye
kushindwa kulipa faini.
Wadau hao, wamemshutumu Mnyalu kuimiliki Tanzanite FC kinyume na
makubaliano ya kuitafutia wafadhili na badala yake kujitangaza kuwa ni
mmiliki baada ya kukabidhiwa leseni na cheti cha usajili wa timu.
Walisema kuwa kutokana na kujitangaza huko, Mnyalu amekuwa akipata
misaada mbalimbali na kujinufaisha kwa mwamvuli wa kuwa mmiliki wa
Tanzanite FC, wakati alikuwa kama mfadhili tu.
Kocha wa timu hiyo, Ally Matimbwa, alisema yeye ndiye mmliki halali
wa timu hiyo, na kosa kubwa walilolifanya ni kumkabidhi Mnyalu timu na
baadaye kuwageuka na kuihodhi moja kwa moja.
“Sisi ndio wamiliki halali wa Tanzanite FC na tulikuwa tunashindwa
kumudu baadhi ya gharama, ambapo tuliamua kutafuta wafadhili na kumpata
Mnyalu. Kosa kubwa tulilofanya ni baadaye kumuamini sana na kumpatia
‘documents’ za timu, hali ambayo sasa anatamba kuwa timu ni yake,”
alisema.
Kwa upande wake, Mnyalu akionyesha kushangazwa na tuhuma hizo,
alisema kuwa kuna baadhi ya watu wanatumika kumchafua baada ya kuona
maendeleo ya Tanzanite FC kutoka wilayani hadi sasa inatisha katika
ngazi ya taifa.
“Hizo ni kelele tu za watu kwa lengo la kunichafua baada ya kuona
timu inapaa angani kutoka wilayani, mkoani na sasa taifa, ndiyo maana
kelele nyingi zinaibuka, ila kama ujuavyo dua la kuku haliwezi kumpata
mwewe, ndivyo hivyo na mimi wala kelele hizo hazitanirudisha nyuma
kuihudumia timu na nazidi kusema kwa herufi kubwa kuwa, mimi ndiye
mmiliki halali wa timu na anayepinga ajitokeze,” alitamba Mnyalu.
Tanzania Daima ilipiga hodi Chama cha Soka Wilaya ya
Simanjiro (SIDFA), ambako Katibu wake, Zefania Simon, alithibitisha
Mnyalu ndiye mmiliki halali wa timu hiyo.
Kutokana na hali hiyo, Zefania alitoa onyo kali kwa watu hao
wanaojiita wamiliki wa timu hiyo na kuwataka kufuata taratibu halali
kwa mujibu wa katiba ya chama, juu ya uhalali huo.
Chanzo:Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment