Home » » WAFUNGWA WADAI KULISHWA CHAKULA KIBOVU.

WAFUNGWA WADAI KULISHWA CHAKULA KIBOVU.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Wafungwa wanaotumikia vifungo mbalimbali katika gereza kuu la Lilungu, mkoani Mtwara, wanakabiliwa na hali ngumu kimaisha kutokana na kupewa chakula kibaya na huduma mbovu za vyoo hivyo kutishia kuanzisha mgomo.
Taarifa ambazo Nipashe imezipata kutoka gerezani humo, zilizoelezwa na wafungwa hao, zilisema tatizo la kupewa chakula kibovu limekuwa la muda mrefu na uongozi wa gereza umekuwa hauchukui hatua kila ukielezwa.
Wafungwa hao (majina tunayo) walibainisha mambo sita wanayolalamikia kuwa ni kupewa chakula kibovu na huduma mbaya za ndani na kwamba hadi sasa bado wanatumia mtondoo na hakuna huduma ya matunda hadi wakati wa msimu wa maembe tu.
Malalamiko mengine ni kukosekana kwa mboga za majani kutokana na bustani ya gereza kubinafsishwa kwa mkuu wa gereza hilo ambaye hulazimika kuuza mboga kwa gereza na kutokuwapo huduma ya nyama ambayo wanapewa mare nne tu kwa mwezi.
Kutokana na hali hiyo, Januari 14, mwaka huu, wafungwa katika gereza hilo walianza mgomo baridi baada ya kupikiwa mchele uliodaiwa kuwa na wadudu (funza).
Walisema malalamiko hayo kila wanapowaeleza viongozi wao wamekuwa wakijibu kuwa ni kwa sababu serikali haijawalipa wazabuni wanaotoa huduma ya chakula.
Ofisa Habari Jeshi la Magereza, Deogratius Kazinja, alipoulizwa alisema ofisi yake bado haijapokea malalamiko ya wafungwa hao na kwamba taarifa rasmi za masuala hayo zinaweza kutolewa na viongozi wa juu wa jeshi. 
Kazinja alisema migomo ya wafungwa imekuwa ikijitokeza mara kadhaa katika magereza lakini haisababishwi na uongozi wa magereza kushindwa kutatua malalamiko yao.
Kwa upande wake, Mkuu wa Magereza Mkoa wa Mtwara, Mussa Kaswaka, alipoulizwa alisema hawezi kuzungumzia malalamiko hayo kwa sababu kwa utaratibu wa jeshi hilo ni hadi apewe ruhsa ya kuzungumza na Kamishna Jenerali wa Magereza.
“Mimi si msemaji wa Jeshi la Magereza. Nenda  makao makuu kaonane na Kamisha Jenerali wa Magereza halafu yeye ndiye atatoa maelekezo kama niyatolee ufafanuzi,” alisema.
Juhudi za kumtafuta Kamishna Jenerali wa Magereza, John Minja, hazikuzaa matunda jana. Hata hivyo Nipashe linaendelea kufanya jitihada za kumtafuta ili kuzungumzia malalamiko hayo.
Migomo katika gereza hilo imekuwa ikijitokeza mara kadhaa mfano mwaka juzi, wafungwa wanaotumikia waliitisha mgomo kushinikiza uongozi wa gereza kuwatendea haki kama binadamu wengine kwa kuwapatia chakula kizuri.
Kipindi hicho wafungwa hao walilalamika kuwa wanalishwa uji wa chumvi, ugali na kunde ambazo hazijaungwa kila siku wakati wanastahili kupewa uji wenye sukari, nyama, maziwa, matunda na mboga kama ratiba ya chakula inavyoonyesha.
SOURCE: NIPASHE.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa