Home » » Wakulima watakiwa kuondoka hifadhini

Wakulima watakiwa kuondoka hifadhini

Mkuu wa Mkoa wa Manyara Elaston MbwiloSERIKALI mkoani Manyara imewataka wakulima walio eneo la hifadhi ya msitu wa jamii ya Embreloy Murtangus, wilayani Kiteto kuondoka kwa hiari yao kabla ya Desemba 27 mwaka huu.
Rai hiyo ilitolewa juzi na Mkuu wa Mkoa wa Manyara Elaston Mbwilo wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisi kwake juu ya mgogoro wa ardhi kati ya wakulima na serikali wilayani humo kugombea eneo la hifadhi ya jamii.
Alisema mgogoro huo ulianza mwaka 2006 ambapo ilionekana hao wavamizi ambao ni wakulima wana haki na ilifikia mahali walishtaki halmashauri ya wilaya na kijiji mahakama ya wilaya na Mahakama Kuu ambako walishinda kesi.
Hata hivyo, wilaya ilikata rufaa Mahakama Kuu ambayo Desemba mwaka jana iliamuru ardhi hiyo irejeshwe kwenye kijiji na halmashauri ni baada ya kuona vijiji viliamua kutoa eneo kwa ajili ya hifadhi.
“Wananchi waliamua kutoa eneo kwa ajili ya kulihifadhi kwa manufaa mbalimbali ikiwemo kuvuna wanyama ambao wapo ndani ya msitu huo, kuweka mizinga ya asali, mbao, huku wafugaji wakifaidika na malisho wakati wa msimu wa ukame,” alisema Mbwilo.
Alisema kabla ya kuzuka kwa mgogoro huo, baadhi ya wakulima kutoka nje ya Mkoa wa Manyara kama mikoa ya Iringa, Dar es Salaam na Dodoma, waliingia ndani ya msitu huo kwa kufanya uharibifu wa kufyeka msitu na kuanza kufanya shughuli za kilimo bila utaraibu huku wengi wao wakijimilikisha sehemu kubwa ya ardhi.
“Mnakumbuka mwaka jana wakulima hao waliandamana na matrekta yao zaidi ya 400 wakimweleza Waziri Mkuu kuwa matrekta hayo walikopa kwa ajili ya kulima kwenye eneo hilo sasa fedha zake watarejeshaje,” alihoji.
Alisema maamuzi ya kuondolewa kwa wakulima ndani ya hifadhi hiyo sio suala la Mkuu wa Mkoa wala Mkuu wa Wilaya bali ni la Mahakama ya Rufaa ambayo ilitoa uamuzi huo.
“Sio suala tena la kusema sisi hatutoki hapa, sisi tutatekeleza maamuzi ya mahakama,” alifafanua Mbwilo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa