Home » » Mahakama kuzindua mpango mkakati wa miaka 5 utakaoboresha utendaji wa Mahakama nchini

Mahakama kuzindua mpango mkakati wa miaka 5 utakaoboresha utendaji wa Mahakama nchini


Na. Abushehe Nondo na Immaculate Makilika- MAELEZO
Jaji Mkuu   wa Tanzania  Mohamed Chande Othman amesema kuwa   Serikali inatarajia kuzindua mpango mkakati  wa Mahakama ya Tanzania kwa miaka 5 unaolenga  kuboresha huduma za kimahakama nchini.
Aidha Jaji Mkuu alisema uzinduzi wa mpango huo utaenda sambamba na mradi wa maboresho wa huduma za utoaji haki nchini uliogharimu kiasi cha Tsh Bilioni 140.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam Jaji Chande alisema kuwa  mradi huo una nguzo tatu ambazo ni utawala bora na uwajibikaji , fursa ya kutoa na kupata  haki na uharakishaji wa mashahuri ambapo kwa pamoja umekusudia kutoa haki kwa wote na kwa wakati.
Katika kujenga imani ya wananchi kwa mahakama tunataka kufikia sehemu ambapo mtu yeyote akileta shauri lake Mahakamani basi litasikilizwa kwa wakati” alisema Jaji Chande.
Aliongeza kuwa taarifa za hivi karibuni zinaonyesha kuwa asilimia 47 ya Watanzania hawana fursa sawa ya kupata haki ya Mahakama katika maeneo waliopo hususani mikoani kwa kuwa mikoa mingi haina Mahakama Kuu, hivyo mpango huo utakaozinduliwa utalenga kuboresha utendaji na utoaji huduma za kimahakama nchini.
Akizungumzia kuhusu mradi wa maboresho ya huduma za Mahakama ambao unaandaliwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania na Benki ya Dunia  Jaji Chande alisema kuwa mradi huo unalenga kuimarisha mifumo ndani ya Mahakama, kuendesha kesi  na utoaji wa hukumu kwa wakati.
Jaji Chande aliongeza kuwa mradi huo utapanua wigo wa utoaji huduma za kimahakama ambapo itatoa fursa za mafunzo endelevu kwa watumishi wa Mahakama 6400 wa ngazi mbalimbali.
Aidha alisema mpango huo utasaidia kuimarisha Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa  kukijingea uwezo wa kutoa taaluma bora kwa watumishi pamoja na wadau katika masuala ya Sheria.
Jaji Chande alisema tayari mradi huo umewezesha kujengwa kwa Mahakama tano za kisasa zilizopo katika maeneo ya Kibaha, Kawe, Kisarawe, Kigamboni na  Bagamoyo ambazo zitakuwa mfano wa uanzishwaji wa Mahakama za kisasa nchini.
Mradi huo unaogharimu bilioni 140 utazinduliwa Kibaha mkoani Pwani  Septemba 21 mwaka huu, ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Manyara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa